Chama cha Wananchi (CUF) Kutoa Tamko Zito Kuhusu Hatima yake Kisiasa Zanzibar...Maalim Seif Apunguziwa Ulinzi | KINGAZI BLOG

KARIBU UHABARIKE KIGANJANI MWAKO.

Breaking News
Loading...

Monday, March 28, 2016

Chama cha Wananchi (CUF) Kutoa Tamko Zito Kuhusu Hatima yake Kisiasa Zanzibar...Maalim Seif Apunguziwa Ulinzi


Chama cha Wananchi (CUF), kimesema kinajiandaa kutoa tamko zito kuhusu hatima yake kisiasa visiwani Zanzibar.
Kufuatia hatua ya Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zaniabar (ZEC), Jecha Salum Jecha kufuta Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana, ambao chama hicho kinaamini kuwa kilishinda, CUF iligomea uchaguzi wa marudio wa Jumapili iliyopita.
Tangu hapo, Rais Dk. Ali Mohammed Shein alishaapishwa Alhamisi iliyopita kuongoza visiwa hivyo mpaka mwaka 2020.
CUF inaamini matokeo ya uchaguzi wa mwaka jana yangeonyesha kuwa mgombea wao, Maalim Seif Hamad, ameshinda kwa kishindo.
Aidha, Chama hicho kimesema hakitababaishwa na hatua ya serikali kumwondolea walinzi Maalim Seif  kwasababu chama hicho kina walinzi wa kutosha kufanya kazi hiyo .
Akizungumza na Nipashe jana, Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Bara, Magdalane Sakaya, alisema CUF inafanya maandalizi ya vikao vya ngazi za juu ambavyo ndivyo vitakavyotoa maamuzi kuhusu mustakabali wa kisiasa visiwani humo, baada ya uchaguzi wa marudio.
Sakaya ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Kaliua mkoani Tabora kwa tiketi ya CUF, alisema ingawa shughuli za chama zinaendelea kama kawaida, vikao hivyo ambavyo ni Kamati Tendaji na Baraza Kuu vitakaa ndani ya muda mfupi ujao na vitajadili na kutoa msimamo wa chama kuhusu hatma ya Zanzibar.
“Tunaendelea na maandalizi ya vikao hivyo na wiki ijayo vitakaa na kutoa mwelekeo wa nini kinaendelea na nini msimamo wa chama kuhusu siasa za Zanzibar, lakini tunaendelea kuamini kuwa mgombea wetu ndiye chaguo sahihi la Wazanzibari katika uchaguzi wa Oktoba 25 mwaka jana,” alisema Sakaya.
Aidha, Sakaya alisema CCM ilishapanga siku nyingi za kuhakikisha wanashinda kwa hila kwenye uchaguzi huo ili wabadili Katiba ya Zanzibar inayozungumzia Serikali ya Umoja wa Kitaifa na hatimaye waunde serikali peke yao ambayo haitakuwa na vyama vya upinzani.
Kuhusu taarifa za Maalim Seif kupunguziwa walinzi, Sakaya alisema CUF haiwezi kubababishwa na hilo kwasababu chama chao kina walinzi wa kutosha ambao watamlinda wakati wote na aliongeza kuwa hatua ya CCM kulazimisha kumwapisha Dk. Shein ni udikteta wa kupindukia.
Alielezea kushangazwa na idadi kubwa ya askari polisi na wa JWTZ wakati wa uchaguzi wa marudio, hali ambayo iliwatisha wananchi na wengine kuogopa kwenda kwenye shughuli zao za kila siku.
“Baadhi ya wanachama wa CUF bado wako mahabusu hadi leo na wanasheria wetu wanaendelea na mchakato wa kuwatoa maana hawana kesi," alisema Sakaya.
"Wengi walipigwa na kuteswa na kubambikiwa kesi kwasababu za kisiasa na kwa kuwa wameshatimiza kile walichokuwa wanakitaka tunaamini watawaachia.”
Mwenyekiti wa ZEC Jecha alimtangaza Dk. Ali Mohammed Shein kuwa Rais wa Zanzibar Jumatatu kwa kupata asilimia 91.4 ya kura halali.
Kwa mujibu wa Jecha, Shein alipata kura 299,982 kati ya jumla ya wapiga kura waliojitokeza 341, 865. Jumla ya Wazanzibari wlaiojiandikisha walikuwa kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana ambao ulifuntwa na Jecha walikuwa 503,580.
Nafasi ya pili ilichukuliwa na mgombea urais wa ADC, Hamad Rashid aliyepata kura 6,734 na Maalim Seif Sharif Hamad (CUF) alishika nafasi ya tatu kwa kupata kura 6,076.
Ushindi wa Dk. Shein wa asilimia 91.4 una maana vyama vingine saba vilivyoshiriki vilikosa asimilia 10, ambazo kisheria zingeliweza kukifanya kuingia kwenye serikali ya umoja wa kitaifa.
Jecha aliufuta uchaguzi wa Oktoba 25 kwa madai ya kuwepo kasoro kubwa, hatua ambayo ilipingwa vikali na CUF, ambacho aliyekuwa mgombea wake wa urais, Maalim Seif Sharif Hamad, alisema alikuwa ameshinda kwa zaidi ya 52%.
Bado haijafahamika ikiwa Dk. Shein ataunda serikali nyengine yenye muundo wa umoja wa kitaifa, kwasababu  mbali na chama chake, hakuna chama kingine kilichotangazwa na ZEC kufikia asilimia 10 ya kura za jumla wala kupata wajumbe kwenye baraza la wawakilishi, masharti muhimu kwa chama kujumuishwa kwenye uundaji wa serikali kwa mujibu wa katiba ya visiwa hivyo.

google+

linkedin

About Author
  • BLOG NAMBA MMOJA KWA MATANGAZO YA AJIRA NA NAFASI ZA KAZI TANZANIA. Soma zaidi

     

    Gallery

    Popular Posts

    About Us