Majambazi mipaka ya Kenya, Tanzania wauawa | KINGAZI BLOG

KARIBU UHABARIKE KIGANJANI MWAKO.

Breaking News
Loading...

Saturday, March 26, 2016

Majambazi mipaka ya Kenya, Tanzania wauawa



WATU sita, wakiwemo wanne wanaosadikiwa kuwa majambazi hatari katika mipaka ya Tanzania na Kenya, wameuawa katika mji wa Isebania, Kenya wakati wa uporaji fedha kutoka duka la mfanyabiashara wa vifaa vya ujenzi katika eneo la
Isebania.
Mbali na mauaji hayo, pia askari Polisi Kituo cha Isebania, wamefanikiwa kukamata bunduki 2 aina za AK 47, zilizotumiwa na majambazi katika uporaji wa fedha katika duka hilo mali ya Saiya Mgendi.
Akizungumza katika mji huo juzi, Mwenyekiti wa Haki za Binadamu Wilaya ya Kurya West ya Kenya, Peter Masaithe alisema watu hao wanne waliouawa, wanashukiwa ndio waliokuwa wakijihami kwa bunduki hizo.
Alidai kuwa juzi saa 10:30 jioni, kundi hilo la majambazi walivamia duka la mfanyabiashara wa vifaa vya ujenzi na kushambulia mke wa mwenye duka na mfanyakazi wake, wakilazimisha kupatiwa fedha ambapo kwa muda mfupi, walifanikiwa kupora fedha ambazo kiasi chake hakijajulikana zikiwemo fedha za Kenya na za Tanzania.
Alisema majambazi hao walifyatua risasi hewani kutishia wananchi waliotaka kujitokeza kutoa msaada kwa walioporwa fedha, ndipo askari wa Isebania waliokuwa doria maeneo hayo na wananchi wakajitokeza kwa wingi kutoa msaada, wakashirikiana na wananchi wengine kutoka upande wa Sirari kuwasaka.
Hata hivyo katika mapambano hayo, alisema wananchi wawili walioshiriki kutafuta majambazi hao, akiwemo kijana aliyekuwa akichunga ng’ombe aliyejaribu kuwaelekeza wananchi walikojificha majambazi hao na mmoja wa waliokuwa wakiwatafuta, walipigwa risasi na kufa papo hapo.
Wakati wa mapambano hayo wananchi walihamasishana kwa kusema, “Wanaume wote hakuna kurudi nyuma hadi kieleweke sisi na majambazi ama zao ama zetu wamezoea kutufilisi na kutuua tuungane kama Watanzania wanavyofuata nyayo kwa pamoja kwa kujitokeza bila kurudi nyuma tutafanikiwa kukomesha ujambazi huu wa mchana na usiku hawa majambazi wametuzoea miji ya Isebania na Sirari,” walisikika wakisema.
Diwani wa Kata ya Sirari, Nyangoko Paulo na wananchi wa mji wa Sirari, Tarime wamewapongeza wananchi wa mipakani na Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na kuwatokomeza majambazi hao na bunduki mbili kukamatwa, ikiaminika walikuwa hatari kwa usalama wa mali na raia wa vijiji vya mipaka ya Kenya na Tanzania.
Wahalifu wengi wanaotumia silaha za moto wanadaiwa kutokea Vijiji vya Masangura, Kegonga, Nyametaburo na Nyomutiro kwa upande wa Kenya na kwa upande wa Tanzania wengi hutokea Vijiji vya Kebeyo tarafa ya Inchugu, Mriba, Kegonga, Gibaso, Nyakunguru vya Tarafa ya Ingwe.

google+

linkedin

About Author
  • BLOG NAMBA MMOJA KWA MATANGAZO YA AJIRA NA NAFASI ZA KAZI TANZANIA. Soma zaidi

     

    Gallery

    Popular Posts

    About Us