Serikali ya Magufuli inazingatia uadilifu, uaminifu na uwajibikaji | KINGAZI BLOG

KARIBU UHABARIKE KIGANJANI MWAKO.

Breaking News
Loading...

Tuesday, March 15, 2016

Serikali ya Magufuli inazingatia uadilifu, uaminifu na uwajibikaji



HAKUNA shaka kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imevutia wengi katika muda wa takribani miezi minne ambayo imekuwa madarakani. Watanzania wengi wamekuwa na imani kubwa na Serikali ya
Rais John Magufuli, baada ya kuanza kazi kwa kishindo huku ikifanya mambo ambayo huko nyuma ilionekana kwamba yana ugumu kufanyika.
Chini ya Rais Magufuli na kaulimbiu yake ya ‘Hapa Kazi Tu,’ Serikali ya Awamu ya Tano imeonesha kwa vitendo, kupambana na maovu hususani ubadhirifu, wizi, uzembe na njama za kuhujumu mapato ambapo wakati wa kuzindua Bunge la Kumi na Moja, Dk Magufuli, alifananisha mapambano hayo na utumbuaji wa majipu.
Alifafanua kwamba ingawa majipu yanauma, lakini njia sahihi ya kuyaponesha ni kuyatumbua. Tangu waanze kazi hiyo ya kurejesha maadili katika utumishi wa umma, wananchi wameridhishwa na kazi hiyo ya viongozi wa Serikali ya Tano inayoongozwa na Rais Magufuli na msimamizi mkuu wa shughuli za Serikali, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye sasa huko mitaani anajulikana kama ‘Mzee wa Kutumbua Majipu’ au ‘Mzee wa Bandari.’
Wananchi wanafurahiswa jinsi Rais Magufuli na timu yake wanavyofanyakazi ya kurudisha nidhamu kwa watumishi wa umma bila kumuonea haya mtu yeyote. Ndiyo maana kwa watumishi wa umma sasa kila mmoja yuko roho juu anaposikia Waziri Mkuu, Majaliwa anatembelea eneo lao la kazi, kiasi wengine kueleza kuwa ni heri kukutana na Rais Magufuli kuliko Majaliwa.
Kwa siku tano kuanzia Machi 2, mwaka huu, Waziri Mkuu, Majaliwa alikuwa katika ziara ya kikazi mkoani Simiyu, na hali ilionekana dhahiri kuwa watumishi wengi wa umma walikuwa roho juu wakihisi kuna utumbuaji wa majipu. Hata Mkuu wa Mkoa huo, Eraston Mbwilo amekiri mbele ya Waziri Mkuu kwamba alikuwa na wasiwasi baada ya kusikia anatembelea mkoa wake, tena siku chache baada ya kutoka Mtwara ambako ‘alimtumbua’ daktari aliyedai rushwa ya Sh 100,000 ili afanye upasuaji kwa mgonjwa.
“Kwa kweli hata mimi nilikuwa na wasiwasi nilipoambiwa Waziri Mkuu anakuja kwangu, tena wakati akitokea Mtwara ambako alikuwa ametumbua watu. Nilijiuliza moyoni kuna usalama kweli?” alisema Mbwilo wakati wa mkutano wa watumishi wa umma na Waziri Mkuu wilayani Meatu, Machi 5, mwaka huu. Kauli kama hiyo ya kuonesha wasiwasi siyo tu ilitolewa na mkuu wa mkoa, lakini hata wabunge akiwamo wa Meatu, Salum Khamis Salum ‘Mbuzi’ aliyesema watumishi wa umma hapo walikuwa na hofu juu ya ziara ya Waziri Mkuu, lakini akaongeza kuwa wilaya hiyo haina majipu, na kuwaondoa hofu watumishi kuwa hawatatumbuliwa.
Hofu ya watumishi wa umma ni dhahiri kutokana na ukweli kuwa Waziri Mkuu Majaliwa ameshiriki katika utumbuaji wa majipu mengi tangu ashike wadhifa huo akiwa kiranja mkuu wa kusimamia utendaji kazi serikalini. Na katika ziara zake hizo za mikoani, anazidi kuwatia hofu watumishi kwa sababu kila anapokwenda, anaomba kukutana na watumishi wa umma iwe kabla ya kuzungumza katika mikutano ya hadhara na wananchi au baada ya kuzungumza na wananchi hao.
Lakini lililowazi na ambalo Waziri Mkuu, Majaliwa huliweka wazi kwa watumishi hao wa umma ni kwamba amefika kwao siyo kutumbua majipu, bali kueleza kile ambacho Serikali ya Awamu ya Tano inakitarajia kutoka kwa watumishi hao wa umma kote nchini. Kwa mujibu wake, kubwa ni katika kuhakikisha kuwa Watanzania wenzao wanahudumiwa vizuri wanapofika katika ofisi za serikali na wanaridhika na huduma hizo.
Anasema jukumu kubwa la watumishi wa umma sasa ni kufanyakazi kwa bidii na kuisaidia Serikali ya Awamu ya Tano katika kukabiliana na changamoto mbalimbali. Anasema kila mtumishi katika eneo lake atambue kuwa serikali inachotaka ni kuona huduma kwa wananchi zinaimarika na hakuna usumbufu wakati wa kupatiwa huduma hizo. “Mfanye kazi zenu kwa usahihi na kuhakikisha mnatoa huduma nzuri kwa wananchi.
Tunataka kila mwananchi aone hii ni serikali yake, akifika ofisi ya serikali apokelewe, asikilizwe na ahudumiwe vizuri. Na hata kama amekuja kwako kimakosa, muelekeze kwa kumpeleka ofisi husika,” anasema Majaliwa. Anasema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inataka watumishi wa umma wawe waadilifu, waaminifu na wanaowajibika kwa wananchi.
Anasema watumishi hao lazima wawe na huruma na kwamba wamesomeshwa na wana utaalamu ambao unahitajika kuwatumikia Watanzania wenzao, na siyo kujisifu kwa elimu zao badala ya kuleta matokeo. “Tupo kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania, tuna mtihani mzito, wasipoona mafanikio watasema ‘si unaona wanavaa suti nzuri, wanatembelea magari kwa kodi zetu lakini hawafanyi chochote,” anasema Majaliwa.
Anaendelea kusema: “Kuwahudumia ndio mtihani wetu… Wahudumieni watu wetu, msipofanya vizuri mtaipaka doa serikali nzima.” Majaliwa anawataka watumishi wa Serikali kuwa wavumilivu wakati madeni yao yanashughulikiwa na kusisitiza kuwa madeni yao kwa serikali yasiwe chanzo cha kuwaadhibu wananchi kwa kuwanyima huduma na kuomba rushwa. “Madeni yenu yasiwe chanzo cha kuwaadhibu wananchi kwa kuwanyima huduma… Tafadhali msichukue rushwa mtaharibu kazi yenu,” Majaliwa anasisitiza.
Katika kusisitiza hilo, alirejea mifano miwili; daktari wa Hospitali ya Mkoa wa Mtwara ya Ligula aliyedaiwa kumwomba rushwa ya Sh 100,000 mkazi mmoja wa mkoani humo ili baba yake afanyiwe upasuaji, na tukio la muuguzi wa Hospitali ya Butimba Nyamagana mkoani Mwanza, kuzembea na kusababisha mjamzito kupoteza pacha wakati akijifungua. “Serikali hii haitawafumbia macho watumishi wasio waadilifu, waaminifu na wasiowajibika.
Hatutahamisha mtumishi mzembe kutoka Bariadi kwenda Bunda, tutamfukuza kazi. “Tutamalizana naye na shughuli yake itakuwa imeishia hapo,” Majaliwa anaeleza na kusisitiza kuwa huo ndio utaratibu wa Serikali ya Awamu ya Tano. Anaendelea kusema, “Hatutamwonea mtu yeyote, msiwe na hofu, mwenye hofu ni yule mwenye matatizo.”
Amerejea kauli yake kuwa serikali inatambua inadaiwa na watumishi wa umma na inafanya jitihada za kumaliza malimbikizo ya madeni hayo, na pia kuweka mifumo ambayo haitazalisha tena malimbikizo. “Tuna hakika tutafanikiwa kumaliza malimbikizo hayo na hasa wakati huu ambao makusanyo ni mazuri. Msikiuke miiko ya utumishi eti kwa sababu unaidai serikali… Hasira hasara,” anasema Waziri Mkuu.
Amewaagiza wakuu wa mikoa na wilaya kote nchini kuhakikisha wanasimamia utendaji wa watumishi wa umma ili kuleta tija na ufanisi. Kwa ujumla, watumishi wa umma waadilifu, waaminifu na wanaowajibika hawana haja ya kuwa na hofu na Serikali ya Awamu yaTano, lakini kwa wale wanaotenda kinyume cha haya, ni dhahiri siku zao katika utumishi wa umma zitakuwa zinahesabika.

google+

linkedin

About Author
  • BLOG NAMBA MMOJA KWA MATANGAZO YA AJIRA NA NAFASI ZA KAZI TANZANIA. Soma zaidi

     

    Gallery

    Popular Posts

    About Us