Chama cha Wananchi (CUF), kimesema kinajiandaa kutoa tamko zito kuhusu hatima yake kisiasa visiwani Zanzibar.
Kufuatia
 hatua ya Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zaniabar (ZEC), Jecha Salum 
Jecha kufuta Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana, ambao chama hicho 
kinaamini kuwa kilishinda, CUF iligomea uchaguzi wa marudio wa Jumapili 
iliyopita.
Tangu hapo, Rais Dk. Ali Mohammed Shein alishaapishwa Alhamisi iliyopita kuongoza visiwa hivyo mpaka mwaka 2020.
CUF inaamini matokeo ya uchaguzi wa mwaka jana yangeonyesha kuwa mgombea wao, Maalim Seif Hamad, ameshinda kwa kishindo.
Aidha,
 Chama hicho kimesema hakitababaishwa na hatua ya serikali kumwondolea 
walinzi Maalim Seif  kwasababu chama hicho kina walinzi wa kutosha 
kufanya kazi hiyo .
Akizungumza
 na Nipashe jana, Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Bara, Magdalane 
Sakaya, alisema CUF inafanya maandalizi ya vikao vya ngazi za juu 
ambavyo ndivyo vitakavyotoa maamuzi kuhusu mustakabali wa kisiasa 
visiwani humo, baada ya uchaguzi wa marudio.
Sakaya
 ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Kaliua mkoani Tabora kwa tiketi ya CUF, 
alisema ingawa shughuli za chama zinaendelea kama kawaida, vikao hivyo 
ambavyo ni Kamati Tendaji na Baraza Kuu vitakaa ndani ya muda mfupi ujao
 na vitajadili na kutoa msimamo wa chama kuhusu hatma ya Zanzibar.
“Tunaendelea
 na maandalizi ya vikao hivyo na wiki ijayo vitakaa na kutoa mwelekeo wa
 nini kinaendelea na nini msimamo wa chama kuhusu siasa za Zanzibar, 
lakini tunaendelea kuamini kuwa mgombea wetu ndiye chaguo sahihi la 
Wazanzibari katika uchaguzi wa Oktoba 25 mwaka jana,” alisema Sakaya.
Aidha,
 Sakaya alisema CCM ilishapanga siku nyingi za kuhakikisha wanashinda 
kwa hila kwenye uchaguzi huo ili wabadili Katiba ya Zanzibar 
inayozungumzia Serikali ya Umoja wa Kitaifa na hatimaye waunde serikali 
peke yao ambayo haitakuwa na vyama vya upinzani.
Kuhusu
 taarifa za Maalim Seif kupunguziwa walinzi, Sakaya alisema CUF haiwezi 
kubababishwa na hilo kwasababu chama chao kina walinzi wa kutosha ambao 
watamlinda wakati wote na aliongeza kuwa hatua ya CCM kulazimisha 
kumwapisha Dk. Shein ni udikteta wa kupindukia.
Alielezea
 kushangazwa na idadi kubwa ya askari polisi na wa JWTZ wakati wa 
uchaguzi wa marudio, hali ambayo iliwatisha wananchi na wengine kuogopa 
kwenda kwenye shughuli zao za kila siku.
“Baadhi
 ya wanachama wa CUF bado wako mahabusu hadi leo na wanasheria wetu 
wanaendelea na mchakato wa kuwatoa maana hawana kesi," alisema Sakaya.
"Wengi
 walipigwa na kuteswa na kubambikiwa kesi kwasababu za kisiasa na kwa 
kuwa wameshatimiza kile walichokuwa wanakitaka tunaamini watawaachia.”
Mwenyekiti
 wa ZEC Jecha alimtangaza Dk. Ali Mohammed Shein kuwa Rais wa Zanzibar 
Jumatatu kwa kupata asilimia 91.4 ya kura halali.
Kwa
 mujibu wa Jecha, Shein alipata kura 299,982 kati ya jumla ya wapiga 
kura waliojitokeza 341, 865. Jumla ya Wazanzibari wlaiojiandikisha 
walikuwa kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana ambao 
ulifuntwa na Jecha walikuwa 503,580.
Nafasi
 ya pili ilichukuliwa na mgombea urais wa ADC, Hamad Rashid aliyepata 
kura 6,734 na Maalim Seif Sharif Hamad (CUF) alishika nafasi ya tatu kwa
 kupata kura 6,076.
Ushindi
 wa Dk. Shein wa asilimia 91.4 una maana vyama vingine saba 
vilivyoshiriki vilikosa asimilia 10, ambazo kisheria zingeliweza 
kukifanya kuingia kwenye serikali ya umoja wa kitaifa.
Jecha
 aliufuta uchaguzi wa Oktoba 25 kwa madai ya kuwepo kasoro kubwa, hatua 
ambayo ilipingwa vikali na CUF, ambacho aliyekuwa mgombea wake wa urais,
 Maalim Seif Sharif Hamad, alisema alikuwa ameshinda kwa zaidi ya 52%.
Bado
 haijafahamika ikiwa Dk. Shein ataunda serikali nyengine yenye muundo wa
 umoja wa kitaifa, kwasababu  mbali na chama chake, hakuna chama kingine
 kilichotangazwa na ZEC kufikia asilimia 10 ya kura za jumla wala kupata
 wajumbe kwenye baraza la wawakilishi, masharti muhimu kwa chama 
kujumuishwa kwenye uundaji wa serikali kwa mujibu wa katiba ya visiwa 
hivyo.
