
Chama cha Walimu Tanzania (CWT) Mkoa wa Mwanza kimeunda kamati 
kuchunguza tuhuma dhidi ya baadhi ya walimu wa Shule ya Sekondari Mihama
 wilayani Ilemala kujamiiana na wanafunzi wao. 
Mwenyekiti wa CWT
 mkoani hapa, Sibora Kisheri alisema wameunda kamati hiyo baada walimu 
wanane, akiwamo mkuu, Joseph Marifedha kusimamishwa kazi kwa amri ya 
aliyekuwa Mkuu wa mkoa huo, Magessa Mulongo kwa tuhuma hizo. 
“Haiingii
 akili kuona walimu wote wakawa na sifa ya makosa yanayofanana, hivi 
hakuwapo hata mmoja aliyeshtukia mchezo huo na kuwashauri wezake,” 
alisema Kisheri. 
Alisema uchunguzi huo unalenga kubaini kiini 
cha tuhuma hizo na kuishauri Serikali na vyombo husika hatua stahiki za 
kuchukua kuhakikisha kila upande unatendewa haki. 
Aliwaasa walimu kufuata sheria, kanuni na misingi ya kazi kwa kutimiza wajibu na kuepuka mambo yanayokinzana na taaluma hiyo. 
Hivi karibuni Mulongo aliwasimamisha walimu hao baada ya kupata taarifa kuwa walikuwa wakijihusisha na vitendo hivyo.